TANZANIA KUSHIRIKI MKUTANO WA 81 CISM NCHINI MONACO

Mkutano Mkuu na Kongamano la 81 la Baraza la Michezo ya Majeshi Duniani International Military Sports Council umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha majeshi duniani kupitia michezo, huku hafla rasmi ya ufunguzi iliyofanyika tarehe 4 na 5 Mei 2026 katika Principality of Monaco ikiweka historia kwa kuwakutanisha viongozi na wadau wa michezo ya kijeshi kutoka mataifa 81 duniani. Baada ya siku tatu za mikutano ya maandalizi, kongamano hilo liliingia katika hatua ya shughuli rasmi na za wazi kwa umma, likisisitiza misingi ya mazungumzo, ushirikiano na kaulimbiu ya “Urafiki Kupitia Michezo” ambayo imekuwa dira ya International Military Sports Council tangu kuanzishwa kwake mwaka 1948.

Hafla ya ufunguzi iliyofanyika katika ukumbi wa Salle d’Or ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiongozwa na Waziri wa Nchi wa Monaco Mheshimiwa Christophe Mirmand pamoja na Rais wa International Military Sports Council Kanali Nilton Gomes Rolim Filho, Katibu Mkuu Kapteni wa Jeshi la Wanamaji Roberto Recchia na Makamu wa Rais wa CISM Kanda ya Ulaya Kanali Dirk Schwede. Kongamano hilo linaendelea kujadili maendeleo ya michezo ya kijeshi, kuimarisha diplomasia ya michezo pamoja na kupanga mikakati mipya ya kukuza michezo ndani ya majeshi duniani.

Katika kuendeleza ushiriki wa Tanzania kwenye michezo ya kijeshi kimataifa, Mwenyekiti wa Baraza la Michezo ya Majeshi Tanzania (BAMMATA) Brigedia Jenerali SH Said pamoja na Katibu Msaidizi wa BAMMATA Luteni Kanali Penina Igwe wanashiriki mkutano huo unaoendelea nchini Monaco. Ushiriki wa viongozi hao unaonyesha dhamira ya Tanzania katika kuimarisha ushirikiano wa michezo ya kijeshi kimataifa, kubadilishana uzoefu na kuendelea kuitangaza nchi kupitia michezo. Kupitia International Military Sports Council, majeshi ya dunia yanaendelea kuunganishwa kwa misingi ya urafiki, amani, mshikamano na maendeleo ya michezo badala ya migogoro.

Matukio katika picha

Mwenyekiti wa Baraza la Michezo ya Majeshi Tanzania (BAMMATA) Brigedia Jenerali SH Said pamoja na Katibu Msaidizi wa BAMMATA Luteni Kanali Penina Igwe wanashiriki mkutano huo uliofanyika nchini Monaco

Mwenyekiti wa Baraza la Michezo ya Majeshi Tanzania (BAMMATA) Brigedia Jenerali SH Said pamoja na Katibu Msaidizi wa BAMMATA Luteni Kanali Penina Igwe wanashiriki mkutano huo uliofanyika nchini Monaco