Naibu Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Mhe. Ali Abdulgulam Hussein, amekabidhi rasmi bendera ya Zanzibar kwa timu ya taifa ya Netball wanawake, ikiwa ni ishara ya kuwatakia kila la heri kuelekea ushiriki wao katika Mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki yatakayofanyika nchini Kenya. Hafla hiyo imefanyika katika Makao Makuu ya KVZ, Mtoni Mjini Zanzibar, na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa michezo pamoja na wadau wa sekta hiyo.
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Mhe. Hussein amesisitiza umuhimu wa timu hiyo kuitangaza vyema Zanzibar kimichezo na kuonesha nidhamu, mshikamano pamoja na ari ya ushindi wanapokuwa uwanjani. Amesema kuwa Serikali inaendelea kuunga mkono jitihada za kukuza michezo, hususan kwa timu za wanawake ambazo zimekuwa zikifanya vizuri na kuleta heshima kubwa kwa taifa.
Kwa upande wao, wachezaji wa timu hiyo wameahidi kupambana kwa nguvu zote ili kuhakikisha wanapata matokeo mazuri katika mashindano hayo makubwa ya kikanda. Wamesema maandalizi yao yamekuwa mazuri na wana imani ya kufanya vizuri dhidi ya timu pinzani kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika Mashariki.
Mashindano hayo yanatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa, yakizikutanisha klabu bora kutoka ukanda huu, huku yakiwa ni fursa muhimu kwa wachezaji wetu kuonesha vipaji vyao na kupata uzoefu wa kimataifa. Zanzibar inaendelea kuweka historia katika sekta ya michezo kupitia ushiriki wa timu zake katika mashindano mbalimbali ya kikanda na kimataifa.
Timu ya Taifa ya mchezo wa Mpira wa Pete (Netball) kwenya Hafla ya kukabidhiwa Bendera ya Zanzibar
Pichani ni Mhe. Ali Abdulgulam Hussein, amekabidhi rasmi bendera ya Zanzibar kwa timu ya taifa ya Netball wanawake, ikiwa ni ishara ya kuwatakia kila la heri kuelekea ushiriki wao katika Mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki yatakayofanyika Kenya
Naibu Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Mhe. Ali Abdulgulam Hussein
Luteni Kanali Said A. Shamuhuna